Alibaba

samedi 9 mai 2015

Mja Atafufuliwa Kwa Kitendo Alichofariki Nacho

Hadiyth :

Mja Atafufuliwa Kwa Kitendo Alichofariki Nacho

عَنْ جَابِرٍ (رضي الله عنه) قَال: قَالَ النَّبِيَّ (صلى الله عليه و آله وسلم): ((يُبْعَثُ كُلُّ عَبْدٍ عَلَى مَا مَاتَ عَلَيْهِ)) رواه مسلم

Imepokelewa kutoka kwa Jaabir (رضي الله عنه) ambaye amesema: Mtume (صلى الله عليه وآله وسلم) amesema: ((Kila mja atafufuliwa katika hali aliyofia)).[1]

Mafunzo Na Hidaaya:

    Hima ya kutenda mema na kubakia katika istiqaamah ili kitendo cha mwisho kabla ya kufariki kiwe ni kitendo chema, na kiwe ni kiliwazo siku ya kufufuliwa. [Al-Hijr 15: 99, Al-‘Imraan 3: 102].

الَّذِينَ تَتَوَفَّاهُمُ الْمَلَائِكَةُ طَيِّبِينَ ۙ يَقُولُونَ سَلَامٌ عَلَيْكُمُ ادْخُلُوا الْجَنَّةَ بِمَا كُنتُمْ تَعْمَلُونَ

Ambao Malaika huwafisha katika hali njema watasema: (kuwaambia Waumini): “Salaamun ‘Alaykum (amani iwe juu yenu)! Ingieni Jannah kwa yale mliyokuwa mkitenda”[2]

    Umuhimu wa kupata husnul-khaatimah (mwisho mwema) kabla ya kuaga dunia na sio kuwa katika maasi, khasa pale mtu anapofikia katika umri mkubwa.

    Umuhimu wa kuomba du’aa ya Sunnah: ((Allaahuuma Yaa Muqallibal-Quluub Thabbit Qalbiy 'Alaa Diynik – Ee Allaah Mgeuza nyoyo, Thibitisha  moyo wangu katika Dini Yako))[3], na Du’aa ya Nabii Yuwsuf (عليه السلام (: (([Allaahumma] Anta Waliyyi fid-Duniya wal-Aakhirah, Tawaffaniy Musliman wa-Alhiqniy bis-Swaalihiyn – Ee Allaah, Wewe ni Mlinzi wangu duniani na Aakhirah, Nifishie katika Uislamu na nikutanishe na (waja) wema))[4], ili ajaaliwe mtu kuwa na mwisho mwema kwani ((Allaah Huingia kati ya mtu na moyo wake))[5]. Na hivyo kuna hatari kwa mtu ya kubadilika na kutoweka Iymaan yake. [Hadiyth: ((Mmoja katika nyinyi hufanya vitendo vya watu wa Peponi mpaka baina yake na Pepo ikawa dhiraa na kile kilichoandikwa kikathibiti akafanya ‘amali ya watu wa motoni akaingia motoni. Na mmoja katika nyinyi hufanya ‘amali ya watu wa motoni mpaka baina yake na moto ikawa dhiraa, na hapo kile kilichoandikwa kikathibiti akafanya ‘amali ya watu wa peponi, akaingia peponi))].[6] Na katika riwaaya inayomalizikia: ((…’amali zinahesabika za mwisho)).[7]

    Hatari ya kutenda maasi yakaja kuwa ndio kitendo cha mwisho cha mja, kwani mauti yanamfikia mtu bila ya taarifa, mfano mwenye kusikiliza muziki huku akiendesha gari badala ya kusikiliza Qur-aan.

    Kilicho muhimu ni ‘amali za mwisho, basi atakayefanya ‘amali zake kuwa ni bora katika uhai wake wa mwisho atapata bishara njema na kheri Siku ya Qiyaamah, na atakayefanya maovu katika uhai wake wa mwisho atakutana na shari huko Aakhirah [An-Nahl 16: 97].

    Kutochoka wala kulegea katika kufanya mema na kuacha mabaya kwa kuwa hakuna anayejua wakati gani atatembelewa na Malakul Mawt (Malaika wa kutoa roho).

DALILI ( REFERENCE)

[1]  Muslim.

[2]  An-Nahl (16: 32).

[3]  At-Tirmidhiy na amesema: Hadiyth Hasan.

[4]  Yuwsuf (12: 101).

[5]  Al-Anfaal (8: 24).

[6]  Al-Bukhaariy na Muslim.

[7]  Al-Bukhaariy.

Aucun commentaire:

Enregistrer un commentaire