Alibaba

lundi 12 septembre 2016

TETEMEKO LA WAKALI : Cheki Cristiano Ronaldo alivyomshambulia Hernandez

Madrid ,Hispania. MPAKA soka lao litakapokwisha kabisa miguuni labda ndio tutaachana na ubishi unaoendelea juu ya nani zaidi kati ya Lionel Messi na Cristiano Ronaldo. Sasa ubishi huo umeingia katika hatua mpya baada ya Ronaldo kumshambulia vikali staa wa zamani wa Barcelona, Xavi Hernandez.
Bifu kali la Xavi na Ronaldo limeanzia mapema wiki iliyopita baada ya Xavi, ambaye ni staa wa zamani wa Barcelona aliyecheza na Messi Nou Camp kudai kwamba Ronaldo amekuwa na bahati mbaya kuzaliwa katika kizazi kimoja na Messi.
Xavi alimsifu Ronaldo kwamba ni mchezaji mzuri sana, lakini hapo hapo akaongeza maneno yaliyochochea hasira za Ronaldo kwamba staa huyo wa kimataifa wa Ureno alikuwa na bahati mbaya kuzaliwa katika zama za Lionel Messi ambaye ni nyota wa kimataifa wa Argentina. Mara baada ya pambano la Ligi Kuu ya Hispania La Liga dhidi ya Osasuna waliloshinda 5-2 katika dimba la Santiago Bernabeu, Ronaldo alitumia nafasi hiyo kumbwatukia Xavi ambaye kwa sasa anamalizia maisha yake ya soka Falme za Kiarabu.
“Mchezaji anayeangaliwa sana katika mitandao ni mimi. Wote wanaotaka kutokea kurasa za mbele za magazeti au wanaotaka kufanya promosheni ya vitu inabidi waniongelee mimi,” alisema Ronaldo kwa hasira.
“Ninajali nini mimi ambacho Xavi anasema? Anacheza wapi? Qatar sijui wapi, mimi sijui. Ametwaa kila kitu lakini hajatwaa taji la Mwanasoka Bora wa Dunia. Mimi nimetwaa mara tatu,” alisema Ronaldo ambaye mpaka sasa anatarajiwa kutwaa tena tuzo hizo Januari mwakani baada ya kuipatia Real Madrid ubingwa wa Ulaya msimu uliopita huku akiiwezesha Ureno kutwaa taji la Euro mwaka huu nchini Ufaransa.
Kabla ya hapo Xavi ambaye kama ilivyo kwa wachezaji wengine waliocheza na Messi amekuwa na mapenzi makubwa na staa huyo aliyekulia klabuni kwao akitokea Argentina akiwa mdogo, ndiye aliyeanza kuchochea mambo.
“Ni mjinga tu ndiye ambaye amecheza mpira halafu hatambui kama Ronaldo ni mchezaji mkubwa. Lakini ana bahati mbaya kuzaliwa katika zama moja na Leo,” alisema Xavi wakati alipohojiwa na kituo kimoja cha redio nchini kwao Hispania.
Mpaka sasa mchuano wa mataji kati ya Ronaldo na Messi unaonekana kuwa mkali baada ya Messi kutwaa mataji hayo mara tano huku Ronaldo akitwaa mara tatu ingawa anatazamiwa kutwaa mara ya nne Januari mwakani.
Jumamosi Ronaldo aliifungia bao Madrid akiwa amerudi uwanjani kwa mara ya kwanza baada ya kuumia katika pambano la fainali la michuano ya Euro dhidi ya Ufaransa Julai mwaka huu na tangu hapo alitumia likizo yake ya majira ya joto kujitibu na kujiweka fiti zaidi. Alitumia dakika sita tu kuwakumbusha mashabiki wa soka kuhusu kipaji chake baada ya kufunga bao la kuongoza la Madrid ambayo kwa ushindi huo dhidi ya Osasuna inaifanya timu hiyo bingwa wa Ulaya kushinda mechi zake zote tatu za mwanzo. Limekuwa jambo la kawaida kwa mashabiki wa soka wa Barcelona pamoja na wachezaji waliocheza na Messi au waliowahi kupita Barcelona kutamka hadharani kwamba Messi ni mchezaji bora zaidi kuliko Ronaldo.
Pia limekuwa jambo la kawaida kwa wachezaji wa sasa wa Madrid na mashabiki wao kudai kwamba Ronaldo ni mchezaji bora zaidi kuliko Messi na hivyo kuendeleza vita ya maneno.

Aucun commentaire:

Enregistrer un commentaire