Alibaba

mercredi 19 octobre 2016

Mwanamfalme aliyekiri kuua akatwa shingo Saudi Arabia

Mwanamfalme mmoja nchini Saudi Arabia ameuawa kutokana na makosa ya kumuua mwanamume baada ya mzozo miaka mitatu iliyopita mjini Riyadh, wizara ya mambo ya ndani nchini humo imesema.

Hukumu ya kifo ilitekelezwa dhidi ya mwanamfalme huyo Turki bin Saud al-Kabir katika mji mkuu Riyadh.

Hakuna maelezo zaidi yaliyotolewa kuhusu jinsi alivyouawa, lakini watu wengi waliohukumiwa kifo huuawa kwa kukatwa shingo.
Mwanamfalme huyo ndiye mtu wa 134 kuuawa baada ya kuhukumiwa kifo nchini humo, kwa mujibu wa orodha iliyoandaliwa na shirika la habari la AFP.

Lakini huwa nadra sana kwa watu wa familia ya kifamle kuuawa, wanahabari wanasema.
Mwanamfalme huyo alikiri kumuua raia huyo mwenzake, wizara ya mambo ya ndani imesema kupitia taarifa.
Wizara hiyo imewahakikishia raia kwamba serikali imejitolea "kudumisha usalama na kutekeleza haki".

Taarifa zinasema familia ya marehemu ilikataa malipo ya kifedha kama fidia ili kutoitisha hukumu ya kifo dhidi ya mwanamfalme huyo.
Kisa kinachofahamika zaidi cha mtu wa familia ya kifalme kuuawa ni cha Faisal bin Musaid al Saud, aliyemuua mjomba wake, Mfalme Faisal, mwaka 1975.

Wengi wa wanaouawa Saudi Arabia hupatikana na makosa ya mauaji au ulanguzi wa dawa.
Watu karibu 50 hata hivyo waliuawa siku moja Januari kwa tuhuma za ugaidi, akiwemo mhubiri maarufu wa Kishia Sheikh Nimr al-Nimr.