Alibaba

vendredi 18 novembre 2016

Mwili wa msichana anayetarajia 'kufufuliwa' kuhifadhiwa

Msichana ambaye alitaka mwili wake ugandishwe na kuhifadhiwa kwa matumaini kwamba anaweza kurejeshewa uhai wakati mmoja siku za usoni, alipata ushindi wa kihistoria saa chache baada ya kufariki dunia.

Msichana huyo alitaka mwili wake uhifadhiwe kwenye friji maalum baada ya kufa kwa matumaini kwamba anaweza kurejeshewa uhai, na hata ikiwezekana aponywe, baadaye. Mamake alimuunga mkono lakini babake alikuwa anapinga wazo hilo.

Msichana huyo mwenye umri wa miaka 14 alikuwa anaugua aina nadra sana ya saratani.

Jaji katika mahakama ya Uingereza aliamuru kuwa mama yake ndiye angekuwa na usemi wa mwisho kuhusu mwili wake.

Mwili wa msichana huyo, aliyefariki mwezi Oktoba, sasa umesafirishwa kwa ndege hadi Marekani kuhifadhiwa.

Msichana huyo alikuwa anaishi London na alitumia mtandao wa intaneti kusoma zaidi kuhusu teknolojia ya kuhifadhi miili ya cryonics miezi ya mwisho ya uhai wake.

Matumaini siku za usoni

Cryonics ni teknolojia inayotumia kuuhifadhi mwili kwa kuugandisha kwa matumaini kwamba huenda ikawezekana kuufufua au kupata tiba siku za usoni.

Msichana huyo alimwandikia jaji na kumwambia kwamba alitaka "kuishi muda mrefu" na hakutana "kuzikwa ardhini".
Aliandika: "Nafikiri kuhifadhiwa kwa teknolojia ya cryonic kutanipatia fursa ya kutibiwa na kuamshwa - hata kama ni baada ya miaka mia moja."

Jaji Justice Peter Jackson, alimtembelea msichana huyo hospitalini na anasema aliguswa sana na ujasiri ambao msichana huyo alikuwa nao katika kukabiliana na maradhi aliyokuwa anaugua.

Kwenye uamuzi wake, alisema, uamuzi huo haukuwa kuhusu usahihi au kutofaa kwa cyronics bali mzozo kati ya wazazi wa msichana huyo kuhusu hatima ya mwili wa binti yao.

Mwili kugandishwa

Cryonic ni shughuli ambayo imekuwa na utata mwingi na hakuna ajuaye iwapo inawezekana kufufua miili iliyogandishwa kufikia sasa.

Kuna vifaa Marekani na Urusi ambapo miili inaweza kuhifadhiwa kwenye madini ya naitorjeni kwenye baridi kali (chini ya nyozijoto -130C) - lakini huduma hiyo haipo Uingereza.

Gharama ya kugandisha mwili kwa muda usiojulikana inakadiriwa kuwa takriban £37,000.

------------------------------------------------------

Barua ya msichana kwa jaji

"Nimetakiwa kueleza ni kwa nini nataka jambo hili lisilo la kawaida lifanyike.

"Nina miaka 14 pekee na sitaki kufariki dunia lakini najua nitafariki dunia.

"Nafikiri kuhifadhiwa kwa njia hii ya cyronic kutanipa fursa ya kutibiwa na kuamshwa - hata kama ni miaka mia moja ijayo.

"Sitaki kuzikwa ardhini.
"Ninataka kuishi na niishi muda mrefu na nafikiri siku za usoni huenda kukapatikana tiba ya saratani ninayougua na kuniamsha.

"Ninataka kupata fursa hii.
"Hayo ndiyo mapenzi yangu.
Wazazi wa msichana huyo walitalakiana na msichana huyo hakuwa amekutana na babake kwa miaka sita kabla yake kuanza kuugua.

Mamake aliunga mkono mapenzi yake ya kutaka mwili wake uhifadhiwe kwa kugandishwa lakini babake alikuwa anapinga.

Babake alisema: "Hata kama itawezekana afufuliwe na atibiwe tuseme miaka 200 ijayo, huenda hatapata jamaa yeyote anayemjua na huenda asikumbuke mambo mengi. Atakuwa katika hali ya masikitiko ikizingatiwa kwamba ana miaka 14 na atakuwa Marekani."

Ingawa baadaye alibadili msimamo wake na kusema anaheshimu uamuzi wa bintiye, alitaka kuuona mwili wa bintiye baada ya kifo chake, jambo ambalo msichana huyo alikuwa amekataa.

Jaji alisema ombi la msichana huyo lilikuwa la kipekee kuwahi kuwasilishwa England na Wales, na labda kwingineko.

Kuhitajika kwa sheria

Jaji Jackson alisema kesi hiyo ni mfano wa matatizo mapya yanayoletwa na sayansi kwa wanasheria.
Msichana huyo alifariki Oktoba akifahamu kwamba mwili wake ungegandishwa, lakini jaji alisema kulikuwa na matatizo siku aliyofariki.

Wahudumu wa hospitali na wakuu wao walieleza wasiwasi kuhusu jinsi mwili wake uliandaliwa kwa ajili ya kuhifadhiwa.

Hilo lilifanywa na kundi la watu wa kujitolea Uingereza kabla ya mwili huo kupelekwa Marekani.
Amedokeza kwamba mawaziri wanafaa kutafakari uwezekano wa kutoa kanuni na sheria za kusimamia uhifadhi wa miili kwa kutumia teknolojia ya cyronic siku za usoni.

Shinzo Abe: Nina imani na Donald Trump

Waziri Mkuu wa Japan Shinzo Abe amesema ana imani na Rais Mteule wa Marekani Donald Trump na kwamba wawili hao wanaweza kuaminiana.

Bw Abe ameeleza mkutano wa dakika 90 kati yake na Bw Trump katika jumba la Trump Tower, New York, kama wa uwazi na wa kirafiki.
Wakati wa kampeni, Bw Trump alitilia shaka manufaa ya urafiki kati ya Marekani na baadhi ya washirika wake wa muda mrefu, ikiwemo Japan.

Mkutano huo ulikuwa wa kwanza wa ana kwa ana kati ya Trump na kiongozi wa nchi nyingine duniani tangu ashinde urais.

Marekani na Japan zimekuwa washirika wakubwa tangu kumalizika kwa Vita Vikuu vya Pili vya Dunia, ambapo Marekani iliisaidia Japan kufufua tena uchumi wake.

Trump ameahidi kufuta mktaba wa kibiashara kati ya Marekani na nchi za Pasifiki, ambapo Bw Abe amekuwa wakiuunga mkono sana kama njia ya kukabili ubabe wa kiuchumi wa China.

Mkataba huo uliidhinishwa na bunge la Japan, licha ya uwezekano kwamba huenda ukafutwa Bw Trump atakapoingia madarakani.
Bw Trump pia alisema Japan inafaa kulipia zaidi kwa ajili ya wanajeshi wa Marekani walio kwenye ardhi ya Japan kutoa ulinzi.

Aidha, ametoa pendekezo la Japan na Korea Kusini kustawisha silaha za nyuklia kukabili tishio kutoka kwa Korea Kaskazini.

Mkutano huo inadaiwa ulipangwa baada ya Bw Abe kumpigiakura Trump kumpongeza kwa kushinda uchaguzi wa urais, na kisha akamtajia kwamba angepitia New York akielekea Peru kuhudhuria mkutano wa kibiashara kati ya Asia na nchi za Pasifiki.

Akiongea baada ya mkutano huo, Bw Abe alisema: "Tulikuwa na mazungumzo ya kirafiki na ya kufana sana kwa kipindi kirefu. Yalikuwa mazingira ya kirafiki.
"Ninaamini kwamba bila kuaminiana kati ya nchi hizi mbili ushirikiano wetu hauwezi kufanya kazi siku zijazo na kama matokeo ya mazungumzo yetu leo, nimeshawishika kwamba Bw Trump ni kiongozi ambaye ninaweza kuwa na imani sana naye.

Kiongozi uyo wa Japan hakutoa maelezo mengi kuhusu mkutano huo lakini alisema watakutana tena kujadili kwa kina baadhi ya masuala muhimu.

Katika siku chache baada ya ushindi wake, Bw Trump amezungumza na viongozi kadha wa nchi mbalimbali kwa simu pamoja na baadhi ya watu anaotarajiwa kuwateua kuwa mawaziri katika jumba la Trump Tower.

Mengine yaliyotokea:

   #Luteni Jenerali Mstaafu Michael Flynn amepewa kazi ya kuwa mshauri mkuu wa usalama wa taifa, vyombo vya habari Marekani vimeripoti.

   #Waliomtembelea Trump Tower Alhamisi ni pamoja na waziri wa mambo ya nje wa zamani Henry Kissinger na gavana wa South Carolina Nikki Haley, mmoja wa wanaotarajiwa kupewa kazi ya waziri wa mambo ya nje

   #Mgombea urais wa zamani wa chama cha Republican Mitt Romney atakutana na Bw Trump wikendi hii, kwa mujibu wa vyombo vya habari Marekani

   #Bw Trump atazru majimbo ambayo alishinda kwa mikutano ya kusherehekea ushindi kwa mujibu wa mkurugenzi wake wa kampeni George Gigicos

Kwingineko, makamu wa rais mteule Mike Pence, ambaye pia anaongoza kundi la mpito la Bw Trump amesema ana imani utawala wa Trump utafanya kazi na wafuasi wa chama cha Democratic.

Hayo yakijiri, Rais Barack Obama amemhimiza mrithi wake kuikabili Urusi iwapo itakiuka maadili na sheria za kimataifa.

Baada ya kukutana na Kansela wa Ujerumani Angela Merkel mjini Berlin, Bw Obama amesema anatumai Bw Trump hatakuwa tu mtu wa kucheza siasa na maneno matupu na Urusi.