Alibaba

lundi 23 décembre 2013

DIAMOND,PENNY WAMWAGANA!


Stori: shakoor jongo na mayasa mariwata.
NDIYO habari ya ‘mujini’ kwa sasa, kwamba staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul Juma ‘Diamond Platnumz’ na mwandani wake, mtangazaji wa kituo cha runinga cha DTV, Penniel Mungilwa ‘Penny’ wamemwagana, Risasi Jumamosi limemwagiwa upupu.
Penniel Mungilwa ‘Penny’ na Nasibu Abdul Juma ‘Diamond Platnumz’ wakiwa pamoja katika pozi.
KAMA UTANI, WEMA ATAJWA
Kwa sharti la kutotajwa mahali popote, ‘mtonyaji’ wetu ambaye ni mtu wa karibu wa wawili hao aliliambia gazeti hili kuwa chanzo cha Diamond na Penny kuingia kwenye listi ya ‘zilipendwa’ kilianza kama utani.
Awali ilidaiwa kuwa kila mmoja amekuwa akijiona mwenye thamani mbele ya mwenzake huku Wema Sepetu naye akidaiwa kuwa chanzo.
                                Nasibu Abdul Juma ‘Diamond Platnumz’ akiwa na Wema Sepetu.
“Hakuna penzi tena kati yao, wameachana na kila mmoja yuko kivyake.
“Walianza kama utani, unajua wale kila mmoja anajiona yuko juu kuliko mwenzake, lakini kitendo cha Diamond kuripotiwa kutoka na wanawake tofauti mara kwa mara hasa Wema, kimemchosha Penny ndiyo maana ameamua kujiweka pembeni kuepuka msongamano.
“Kupangwa kama mafungu ya nyanya inahusu?” alihoji ‘kikulacho’ huyo ambaye ni rafiki wa Diamond.

RISASI MZIGONI
Baada ya kutojiridhisha moja kwa moja na taarifa za awali kutoka kwa rafiki huyo, timu ya gazeti hili kwa kuwatumia ‘wahangaikaji’ wake maalum, iliingia mzigoni kupeleleza ukweli juu ya tetesi hizo.
Watu kadhaa walio chini ya Wasafi Classic Baby (WCB) ambayo rais wake ni Diamond walihojiwa ambapo majibu yalikuwa yaleyale kwamba, kwa sasa Diamond na Penny imebaki stori!

 SHAKA ILIPOANZIA
Wakati timu yetu ikiendelea na uchunguzi wake makini juu ya uvumi huo, hivi karibuni Diamond alionekana ‘singo’ kwenye pati ya kusherehekea siku ya kuzaliwa ya ‘dada wa mjini’, Halima Haroun ‘ Halima Kimwana’ ambayo aliiandaa Diamond.
Minong’ono ya kuhoji kutoonekana kwa Penny ilisikika ndani ya Ukumbi wa Business Park, Kijitonyama jijini Dar ilikofanyikia pati hiyo iliyojaa vitendo vya ufuska.
“Haiwezekani leo rais (Diamond) akajiachia peke yake bila Penny. Si kawaida ya Diamond.
“Kwa vyovyote watakuwa wameshamwagana kwa sababu kwenye pati zote huwa wanakuwa pamoja tangu walipoanza uhusiano wa kimapenzi,” alisikika mmoja wa waalikwa katika sherehe hiyo.
Katika tukio hilo, Penny alipigiwa simu na paparazi wetu na kujibu kwa kifupi: “Naumwa. Halafu si lazima nije kwani kila mtu ana ratiba zake.”
                                                                Penniel Mungilwa ‘Penny’.
PENNY KIZIMBANI TENA
Baada ya kukamilisha udadisi huo kupitia kwa watu wao wa karibu, gazeti hili lilianza na Penny kwa kumuuliza undani juu ya habari hiyo lakini alionekana kuwa ‘mzito’ kwa kutoingia ndani kulizungumzia sakata hilo huku akiahidi kulifungukia muda wowote kuanzia sasa.
“Kwa sasa sina cha kuzungumza juu ya hilo, nitalizungumzia muda wowote tena si siku nyingi zijazo, lakini si leo, tafadhali sana,” alijibu Penny kwa kifupi na sauti ya chini iliyojaa uchovu.
Paparazi: “Hebu nisaidie, mko wote au hamko wote?”
Penny: “Nimesema sitoweza kusema lolote kwa leo, subirini.”
                                               Nasibu Abdul Juma ‘Diamond Platnumz’.
DIAMOND KIMYA
Alipotafutwa Diamond kwa njia ya simu yake ya kiganjani, hakupokea licha ya kupigiwa mara kadhaa kwa namba zake zote. Akatumiwa meseji yenye maelezo yote, hakujibu.

MAMA DIAMOND
Ili kujiridhisha na madai hayo, waandishi wetu walimtafuta mama mzazi wa Diamond, Sanura Kassim ‘Sandra’ ambaye alisema hajui na hana taarifa hizo.

NDUGU WA KARIBU SANA
Baada ya mama Diamond, paparazi wetu alimpigia simu ndugu wa karibu sana na Diamond, sikiliza:
Paparazi: “Kumbe Diamond na Penny wamemwagana we huniambii. Sasa wifi yako mpya ni nani?”
Ndugu: “Aka! Sikwambii. Kwanza mi nipo mbali, sipo Dar.

WADAU WANAJUA
Haikuishia hapo, timu yetu ilizungumza na wadau mbalimbali ambao walionesha kusikitika huku baadhi yao wakisema walitabiri tangu awali.
“Duh! Penny ameachia ngazi mwenyewe. Sisi tulijua hawawezi kufika mbali, maana penzi lenyewe lilikuwa na mbwembwe nyingi,” alisema mwanamke mmoja anayejua kila kitu.

TUJIKUMBUSHE
Siku za hivi karibuni Diamond alifanya mahojiano kwa njia ya mtandao mmoja wa kijamii ambapo moja kati ya maswali aliyoulizwa ni pamoja na mpango wa kuoa ambapo alisema kuwa hana mpango huo kwa sasa na hatarajii kumuoa yeyote kati ya wanawake wanaotajwa kwa sana midomoni mwa watu (akiwemo Penny).
Wema alipigiwa simu juzi, lakini simu yake ilikuwa ikiita ‘weee’ mpaka inakatika, inaita ‘weee’ mpaka inakatika.

DAYNA: SITAKI MALUMBANO NA DIAMOND

Na Gladness Mallya
MWANADADA anayetamba na kibao cha Mimi na Wewe, Mwanaisha Said Nyange ‘Dayna’ amefunguka kuwa hataki kabisa kumzungumzia msanii mwenzake, Nasibu Abdul ‘Diamond’.
Mwanaisha Said Nyange ‘Dayna’.
Dayna aliyasema hayo hivi karibuni alipoulizwa kuhusiana na bifu lake na Diamond lililotokana na kumwibia wimbo wake ambapo alisema hataki kumzungumzia kabisa Diamond kwa sababu hataki malumbano kwani hivi karibuni amezungumza maneno mbofumbofu kwenye vyombo vya habari.
Nasibu Abdul ‘Diamond’.
“Mimi sitaki malumbano na Diamond  kwa sababu amekuwa akizungumza mengi sana kwenye vyombo vya habari mengine ya kuniponda na mengine ya kawaida hivyo sitaki malumbano kabisa mimi niko kikazi zaidi yeye aendelee tu”, alisema Dayna.