Alibaba

vendredi 21 octobre 2016

Patrice Evra amaliza ugomvi wake na Luis Suarez

Baada ya kudumu kwa zaidi ya miaka minne, bifu la Patrice Evra na Luis Suarez sasa limefika tamati. Evra amempongeza Suarez baada ya kukabidhiwa kiatu cha dhahabu (European Golden Shoe) kwa kuibuka mfungaji bora barani Ulaya msimu wa 2015/2016

Kupitia akaunti yake ya Instagram, Evra ameandika, “Kwenye Instagram kuna neno upendo tu na hakuna neno chuki !!! Luis, wewe ni mchezaji mkubwa na bora sana, wewe ni namba tisa bora, hongera sana Luis @ luissuarez9. Naupenda sana huu mchezo !!! hahahaah.”

Wawili hao waliingia kwenye ugomvi mzito wakati walipokuwa wakicheza kwenye ligi kuu ya Uingereza huku Evra akiwa Manchester United na Suarez akichezea timu ya Liverpool.

Ugomvi wao ulianza mwaka 2011 wakati wa mechi yao iliyochezwa kwenye uwanja wa Anfield ambapo Evra alidai Suarez alimkashfu kwa maneno ya kibaguzi kitendo ambacho kilisababisha FA kumuadhibu mchezaji huyo kutocheza mechi nane na kulipa faini ya £40,000.

Wachezaji hao walithibitisha kuwa ugomvi wao haushikiki mwaka 2012 wakati wa mechi yao iliyochezwa kwenye uwanja wa Old Traford ambapo Suarez aligoma kumpatia mkono Evra.

Mpango wa kuchezea Uefa Marekani

Rais wa shirikisho la soka la Ulaya (Uefa) amesema bado anafuatilia pendekezo lake la kutaka fainali ya Kombe la Klabu Bingwa Ulaya ichezewe nje ya bara Ulaya.

Aleksander Ceferin, kutoka Slovenia, amesema atafufua tena juhudi zake za kutaka miji iwe ikituma maombi ya kuwa mwenyeji wa fainali hizo.

Amesema anaunga mkono fainali kuchezewa New York.
"Linaweza kuwa wazo tu lakini ni sharti tulizungumzie," amesema Ceferin, ambaye aliteuliwa kuwa mkuu wa Uefa mwezi jana.

Fainali zote 61 zilizochezwa awali zilichezewa Ulaya, lakini Ceferin amesema haliwezi likawa tatizo kwa mashabiki wa soka kusafiri Marekani.
Aliongeza: "Kusafiri kutoka Ureno hadi Azerbaijan kwa mfano ni karibu sawa au ni sawa na kwenda New York."
"Hii ni michuano ya Ulaya kwa hivyo hebu tulifikirie hili."

Kunaweza kuwa na tatizo la nyakati hata hivyo, ikizingatiwa mabadiliko ya saa katika mabara mbalimbali.
Mkuu huyo wa Uefa hata hivyo hana mipango ya kubadilisha wakati wa kuanza kwa fainali, ambayo kawaida huchezwa saa 19:45 BST (20:45 GM).
Fainali zimekuwa zikichezwa Jumamosi tangu 2010.
"Ukiangalia kifedha, hilo haliwezi kufaa. Lakini lazima tufikirie kuhusu masoko mengine pia. China inavutia kama soko, na Marekani pia. Soka inaanza kupata umaarufu huko pia," anasema.